WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene ameongoza mamia ya wakazi wa Dar es Salaam kuaga mwili wa aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sarah Dumba.
Akitoa neno la pole kwa wafiwa jana, kabla ya maziko yaliyofanyika Kigamboni, nje kidogo ya Dar es Salamam, Simbachawene alisema Tanzania imepoteza mtu muhimu ambaye nchi bado ilikuwa inamhitaji kutumikia wananchi.
“ Msiba huu umemuumiza sana Rais John Magufuli na alitamani kushiriki lakini ameshindwa kutokana na kuwepo kwa majukumu ya kitaifa, Dumba ni mtu aliyejituma sana na naamini hata katika uteuzi wa Wakuu wa Wilaya jina lake lingekuwepo kwa sifa nilizozisikia hapa, kwa sababu ndizo Rais anazozitaka, “ alisema Simbachawene.
Alisema ingawa Dumba hayupo tena duniani, watayaenzi yote aliyofanya katika kipindi chote cha uongozi wake. “Hayupo nasi kimwili lakini tutatumia maneno yake na mifano yake kuendelea kuwatumikia wananchi wetu waliotuamini,”aliongeza Simbachawene.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Dk Rehema Nchimbi alisema, mkoa huo umepoteza mtu muhimu aliyejitoa kwa nguvu kubwa kuwasaidia wananchi hususan kwenye eneo hilo. Alisema, Dumba alifanya kazi kwa nguvu zote na kwa upendo na hata kabla ya umauti kumfika, alikuwa akiwatumikia wananchi wake.
“Aliamka asubuhi akiwa hana tatizo lolote na alikwenda kazini kwa ajili ya kuwatumikia wakazi wa Njombe na hata kutoa maagizo kwa viongozi katika ofisi yake. Lakini, ghafla nilisikia amefariki. Imetuumiza lakini kazi ya Mungu haina makosa,” alisema Nchimbi.
Mwenyekiti wa Wakuu wa Wilaya Tanzania, Abdallah Kihato, alisema Dumba alikuwa na msaada mkubwa kwa mambo mbalimbali yaliyokuwa yanawatatiza. Alisema watatumia busara zake kutatua changamoto mbalimbali.
Msiba huo ulihudhuriwa na viongozi wengine mbalimbali wa Serikali, akiwemo aliyekuwa Spika wa Bunge , Ane Makinda, Mbunge na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Mkoa wa Njombe, Deo Sanga, Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Sophia Mjema na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Raymond Mushi.
Dumba alifariki dunia Machi 21 mwaka huu . Kitaaluma alikuwa Mwandishi wa Habari na Mtangazaji wa iliyokuwa Radio Tanzania ambayo kwa sasa inajulikana kama Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC). Alishika nyadhifa mbalimbali za ukuu wa wilaya katika maeneo tofauti zikiwemo wilaya za Kilindi na Njombe mpaka mauti inamfika na ameacha watoto wanne na wajukuu sita.
No comments:
Post a Comment